[Latest Updates]: Mhandisi Samamba Asisitiza Ujenzi wa Viwanda vya Uongezaji Thamani ya Madini Nchini

Tarehe : Oct. 15, 2025, 1:25 p.m.
left

TANGA

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, ametoa wito kwa watendaji wa Tume ya Madini nchini kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya uongezaji thamani ya madini ili kuongeza ajira, kukuza fursa za kiuchumi na kuimarisha mchango wa Sekta ya Madini katika Pato la Taifa.

Akizungumza leo, Oktoba 15, 2025, jijini Tanga katika kikao cha menejimenti ya Tume ya Madini kilichoshirikisha Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, Makamishna wa Tume ya Madini Mhandisi Theonestina Mwasha na Dkt. Theresia Numbi, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, Wakurugenzi, Mameneja na Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, Mhandisi Samamba amesema kuwa Sekta ya Madini ina nafasi kubwa katika kukuza uchumi endapo uongezaji thamani utawekewa kipaumbele.

“Mnapoweka mazingira rafiki ya uwekezaji kama vile kurahisisha upatikanaji wa vibali na miundombinu, wawekezaji wanaongezeka, ajira zinapatikana, mapato ya Serikali yanaongezeka na uchumi unakua,” amesema Mhandisi Samamba.

Amesisitiza Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kushirikiana na viongozi wa mikoa na taasisi nyingine za Serikali kuhakikisha mazingira ya uwekezaji kwenye viwanda vya uongezaji thamani wa madini yanakuwa wezeshi, ili kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.
Katika hatua nyingine, Mhandisi Samamba amewataka Maafisa hao kuendelea kuwajengea uwezo wachimbaji wadogo kwa kuwapatia elimu ya Sekta ya Madini, taarifa za kijiolojia kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), kuwaunganisha na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) pamoja na taasisi za kifedha ili kuongeza tija na mapato yao.

“Ninaamini tukiwasaidia wachimbaji wadogo wataongeza ajira, kukuza mzunguko wa fedha na kuiwezesha Serikali kukusanya kodi zaidi kwa ajili ya kuboresha huduma za kijamii kama elimu, afya, barabara na maji,” amesisitiza.

Aidha, ameitaka Tume ya Madini kuendelea kutoa elimu kwa Chama cha Watoa Huduma kwenye Migodi (TAMISA) ili kuongeza ushiriki wa Watanzania katika Sekta ya Madini kupitia mpango wa Local Content.

Vilevile, amewataka Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kuhakikisha usalama kwenye shughuli za uchimbaji wa madini kwa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara na kutoa elimu ili kuepuka ajali na uharibifu wa mazingira. Pia amesisitiza umuhimu wa kusimamia haki katika utatuzi wa migogoro ya wachimbaji wadogo.

Mhandisi Samamba amehitimisha kwa kuwataka watumishi wote wa Tume ya Madini kushiriki kikamilifu katika zoezi la uchaguzi litakalofanyika Oktoba 29, 2025, nchi nzima.


Kwa upande wao, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo na Katibu Mtendaji, Mhandisi Ramadhani Lwamo, wameishukuru Wizara ya Madini kwa kuendelea kuiwezesha Tume kupitia vitendea kazi ikiwemo magari, pikipiki, fedha na rasilimaliwatu, hali iliyochangia ongezeko la makusanyo ya maduhuli mwaka hadi mwaka.

Wamesema katika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026 (Julai–Septemba), Tume ya Madini imekusanya Shilingi Bilioni 315.4 sawa na asilimia 105.13 ya lengo la Shilingi Bilioni 299.99, na kuwataka Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kuongeza ubunifu na juhudi ili kufikia na kuvuka lengo la Shilingi Trilioni 1.2 kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

by: madini

Latest News
Biteko atoa wito Mabenki ya ndani kuungana kukope…

Waziri wa Madini, Doto Biteko ameyataka Mabenki ya ndani kushirikiana ili kuweza kuzikopesha kampun…

by: madini on: April 23, 2021, 5:11 a.m.

Ukusanyaji wa Maduhuli Sekta ya Madini Wafikia As…

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 202…

by: madini on: April 28, 2021, 12:51 p.m.

Aliyoyasema Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Adol…

’Nimeona Nyuso Zenye Furaha , Amani na Utulivu’’ Ninayo furaha kuwa nanyi hapa ili tuanze safari hi…

by: madini on: Jan. 10, 2022, 2:55 p.m.

Tume ya Madini Yaagizwa Kutafuta Masoko

Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa ameiagiza Tume ya Madini kutafuta Masoko ya wanunuzi wa…

by: madini on: Jan. 30, 2022, 9:32 a.m.

Read News
Contact Us
Permanent Secretary,
Ministry of Minerals,
Madini Street,
Government City, Mtumba
P. O. Box 422,
Dodoma, Tanzania
Email: ps@madini.go.tz
Copyright©2021 Ministry of Minerals