Tarehe : April 15, 2026
TAARIFA YA MHESHIMIWA ANTHONY PETER MAVUNDE (MB.), WAZIRI
WA MADINI KWA VYOMBO VYA HABARI
TAREHE 15 APRILI, 2026
Ndugu Waandishi wa Habari!
Mabibi na Mabwana!
“Jamhuri ya Muungano wa Tanzania”
Ndugu wanahabari, Awali ya yote, ninamshukuru Mwenyezi Mungu, muweza
wa yote kwa kutuwezesha kukutana mahali hapa siku ya leo, tukiwa na afya
njema.
Ndugu wanahabari, Nipo hapa kutoa taarifa ya mambo muhimu kuhusu
uendelezaji wa Sekta ya Madini na mwenendo wa vitendo visivyokubalika kwa
mustakabali wa maendeleo chanya ya Sekta ya Madini hapa nchini.
Ndugu wanahabari, Serikali kupitia Wizara ya Madini inapenda kuujulisha
umma kuwa imeendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa uendelezaji wa
leseni za madini nchini ambapo imebainika kuwepo kwa ongezeko la utoaji wa
leseni za madini nchini, kuna baadhi ya wamiliki wa leseni ambao wamekuwa
hawatekelezi wajibu wao wa umiliki wa leseni ikiwa ni pamoja na
kutokuziendeleza leseni wanazomiliki ndani ya muda uliotolewa kwa mujibu wa
Sheria. Wamiliki hao wamekuwa wanahodhi maeneo; hawalipi ada stahiki za
leseni; hawatekelezi masuala ya Ushirikishwaji wa Watanzania kwenye
shughuli za madini (Local Content), wala Wajibu wa Makampuni kwa Jamii
(Corporate Social Responsibility) vilevile wanashindwa kuthibitisha matumizi ya
fedha yaliyofanyika pamoja na vielelezo vya matumizi husika kwenye
uendelezaji wa leseni hizo.
Ndugu wanahabari, Vitendo vya kuhodhi maeneo vimekuwa vikichangia kwa
kiasi kikubwa kuwepo kwa vitendo vya uchimbaji madini usio rasmi
vinavyotokana na uvamizi wa leseni hizo. Vitendo hivyo havivumiliki na Serikali
itaendelea kuchukua hatua kwa mujibu wa Sheria na kufuta leseni zote ambazo
zitabainika kuwa na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutokuendelezwa
ndani ya muda uliotolewa katika Sheria ya Madini Sura 123.
Ndugu wanahabari, Katika kutekeleza hatua hiyo ya Serikali, leo natangaza
rasmi kufuta leseni 40 za utafutaji madini ambazo wamiliki wake wameshindwa
kuziendeleza licha ya kupewa hati za makosa kutakiwa kurekebisha makosa
yaliyobainika. Aidha, naiagiza Tume ya Madini kufuta leseni hizo na kuendelea
kufanya kaguzi za mara kwa mara za leseni na kuchukua hatua stahiki za
kufuta leseni zote ambazo zitabainika kutokuendelezwa.
Aidha, tarehe 10 Aprili, 2026 Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini imetoa
hati za makosa kwa leseni nyingine 43 zikikujumuisha leseni 40 za utafutaji
madini na leseni tatu (3) za uchimbaji wa kati wa madini. Naielekeza Tume ya
Madini kuendelea na zoezi la utoaji wa hati za makosa na endapo wamiliki
wake watashindwa kurekebisha makosa ndani ya siku 30, leseni hizo
zifutwe ili maeneo hayo yatolewe kwa wawekezaji wengine.
Ndugu wanahabari, pamoja na hatua hiyo, Serikali imeendelea pia kufuatilia
kwa karibu mwenendo wa matukio ya milipuko ya madini ya dhahabu (gold
rush) katika maeneo mbalimbali nchini, na kuchukua hatua stahiki kwa lengo la
kulinda usalama, kudumisha utulivu, na kuhakikisha uzingatiaji wa sheria na
kanuni za madini.
Ni vema ieleweke kuwa, kwa mujibu wa sheria za madini za Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, shughuli zozote za uchimbaji madini zinapaswa
kufanyika kwa kuzingatia umiliki wa leseni halali. Hivyo basi, vitendo vya watu
kukimbilia maeneo yenye taarifa za uwepo wa madini na kuanza uchimbaji bila
leseni ni kinyume cha sheria na havitavumiliwa.
Serikali imekuwa ikichukua hatua za haraka pindi milipuko ya madini
inapojitokeza, ikiwa ni pamoja na:
Kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao;
Kuzuia migogoro kati ya wachimbaji na wamiliki halali wa leseni;
Kulinda mazingira dhidi ya uharibifu unaoweza kusababishwa na
uchimbaji holela;
Kudhibiti hatari za milipuko ya magonjwa ya kuambukiza zinazoweza
kujitokeza katika maeneo ya gold rush.
Katika maeneo ya gold rush, mara nyingi hukusanyika watu wengi kwa muda
mfupi katika mazingira yasiyo rasmi yenye msongamano mkubwa, hali
inayoongeza uwezekano wa kuenea kwa magonjwa ya milipuko. Kutokana na
hali hiyo, Serikali huchukua hatua mahsusi za kiafya, ikiwa ni pamoja na:
Kuratibu uwepo wa huduma za afya za dharura kwa kushirikiana na
mamlaka za afya za maeneo husika;
Kuhamasisha na kusimamia usafi wa mazingira, upatikanaji wa maji
safi na salama pamoja na huduma za vyoo;
Kutoa elimu ya afya kwa wachimbaji na wadau kuhusu kinga dhidi ya
magonjwa ya kuambukiza;
Kufuatilia na kudhibiti magonjwa ya mlipuko yanayoweza kujitokeza,
ikiwemo magonjwa ya mfumo wa hewa, magonjwa ya mlipuko wa
tumbo na mengineyo;
Kuchukua hatua za haraka za kinga na tiba pale dalili za mlipuko wa
ugonjwa zinapobainika.
Ndugu wanahabari, Baada ya hali ya usalama kudhibitiwa, Serikali hufanya
tathmini ya eneo husika, na pale inapobainika kuwa eneo la mlipuko wa madini
halipo ndani ya leseni halali, hatua za urasimishaji huchukuliwa ili kuruhusu
shughuli za uchimbaji kufanyika kwa utaratibu, ikiwemo utoaji wa leseni kwa
wahusika wanaokidhi vigezo.
Hata hivyo, Serikali imebaini kwa masikitiko kuwepo kwa tabia inayoongezeka
ya baadhi ya wachimbaji wadogo wasio waaminifu kuvamia maeneo yenye
leseni halali za madini. Vitendo hivi vimesababisha migogoro, hasara kwa
wawekezaji halali, pamoja na kuvuruga utaratibu wa usimamizi wa sekta ya
madini.
Kutokana na hali hiyo, natoa onyo kali kwa mtu yeyote au kikundi
chochote kinachojihusisha na uvamizi wa maeneo yenye leseni halali kwa
kigezo cha kuifanya kuwa gold rush. Tabia hiyo inakemewa vikali na
kuanzia sasa ni marufuku kuvamia maeneo ya leseni za madini kwa
sababu yoyote ile. Utaratibu wa utoaji wa leseni za madini upo wazi katika
Sheria yetu ya Madini na Kanuni zake na ni lazima ufuatwe.
Serikali haitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wote watakaokiuka
maelekezo haya, ikiwa ni pamoja na kuwaondoa katika maeneo husika na
kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria.
Wizara ya Madini inasisitiza kuwa maendeleo endelevu ya sekta ya madini
yanategemea uzingatiaji wa sheria, nidhamu, na ushirikiano kati ya Serikali,
wawekezaji, na wananchi. Hivyo, wadau wote wanahimizwa kufuata taratibu
zilizowekwa na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani, afya ya jamii,
na utulivu wa nchi yetu.
Ndugu wanahabari, Kwa kumalizia, naomba nitoe rai kwa wawekezaji wote
kwenye Sekta ya Madini kuendelea kuzingatia matakwa ya Sheria ya Madini,
Sura 123. Wizara ya Madini itaendelea kuwapa ushirikiano wawekezaji wote wa
ndani na nje ya nchi wenye nia ya kufanya uwekezaji wenye tija na kukuza
uchumi wa Taifa letu kutokana na uvunaji wa rasilimali madini.
“MADINI NI MAISHA NA UTAJIRI”
“ASANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA”
4
by: madini
Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa ameshiriki Mkutano wa Pili wa Mawaziri wa Madini Afrika …
by: madini on: Oct. 7, 2022, 11:20 a.m.
’Nimeona Nyuso Zenye Furaha , Amani na Utulivu’’ Ninayo furaha kuwa nanyi hapa ili tuanze safari hi…
by: madini on: Jan. 10, 2022, 2:55 p.m.
The Ministry of Minerals informs the public and mining sector stakeholders that Tanzania, in collab…
by: madini on: Jan. 24, 2024, 7:59 p.m.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 202…
by: madini on: April 28, 2021, 12:51 p.m.